Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Kimataifa la Ahlul-Bayt (AS) -ABNA-, Wanafunzi wa Kike wa Jamiatul Mustafa walishiriki katika majlisi ya maombolezo ya mwezi mtukufu wa Muharram iliyofanyika Jumatano, tarehe 17 Juni 2026, katika Msikiti wa Amirul Muuminin (AS), uliopo Magomeni, Dar es Salaam.
Majlisi hiyo ilihudhuriwa na jumla ya wanafunzi 144 wa Jamiatul Mustafa, wakiongozana na msimamizi wao. Hafla hiyo ilipambwa na muhadhara wa Sayyid Hujjatul Islam wal-Muslimin Aidarus, aliyesisitiza umuhimu wa kusimama katika njia ya haki, uadilifu na kujitolea kwa ajili ya kulinda mafundisho ya Uislamu, kwa kufuata mfano wa Imam Hussein (AS).
Mbali na kusikiliza muhadhara, wanafunzi walishiriki katika kisomo cha Qur'ani Tukufu na kuomboleza kwa kusoma qasida na nyimbo za maombolezo ya Imam Hussein (AS), wakionesha mapenzi na mshikamano wao kwa Ahlul-Bayt (AS) katika mwezi huu wa huzuni.
Shughuli hiyo imeendelea kuimarisha malezi ya kiroho na kuongeza uelewa wa wanafunzi kuhusu malengo ya mapinduzi ya Karbala, yanayohimiza kusimama dhidi ya dhulma na kutetea haki katika kila zama.
Your Comment